Zaburi 81

Neno: Kiswahili Contemporary Version

1Mwimbieni kwa furaha, Mungu aliye nguvu yetu; mpigieni kelele za shangwe Mungu wa Yakobo!

2Anzeni wimbo, pigeni matari, pigeni kinubi na zeze kwa sauti nzuri.

3Pigeni baragumu za pembe za kondoo dume wakati wa Mwandamo wa Mwezi, na wakati wa mwezi mpevu, katika siku ya Sikukuu yetu;

4hii ni amri kwa Israeli, agizo la Mungu wa Yakobo.

5Aliiweka iwe kama sheria kwa Yosefu alipotoka dhidi ya Misri, huko tulikosikia lugha ambayo hatukuielewa.

6Asema, “Nimeondoa mzigo mabegani mwao; mikono yao iliwekwa huru kutoka kwenye kikapu.

7Katika shida yako uliniita nami nikakuokoa, nilikujibu katika mawingu yenye ngurumo; nilikujaribu katika maji ya Meriba.

8“Enyi watu wangu, sikieni, nami nitawaonya: laiti kama mngenisikiliza, ee Israeli!

9Hamtakuwa na mungu mgeni miongoni mwenu; msimsujudie mungu wa kigeni.

10Mimi ni Bwana Mungu wako, niliyekutoa nchi ya Misri. Panua sana kinywa chako nami nitakijaza.

11“Lakini watu wangu hawakutaka kunisikiliza; Israeli hakutaka kunitii.

12Basi niliwaacha katika ukaidi wa mioyo yao wafuate mashauri yao wenyewe.

13“Laiti kama watu wangu wangalinisikiliza, kama Israeli wangalifuata njia zangu,

14ningaliwatiisha adui zao kwa haraka, na kuugeuza mkono wangu dhidi ya watesi wao!

15Wale wanaomchukia Bwana wangalinyenyekea mbele zake, na adhabu yao ingedumu milele.

16Bali ninyi mngalilishwa ngano iliyo bora, na kuwatosheleza kwa asali itokayo kwenye mwamba.”

Zaburi

Open the interactive reader to switch translations, adjust type, and mark verses — or browse verses by topic.

Neno: Bibilia Takatifu — Kiswahili Contemporary Version. Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015 Biblica, Inc. Used under the Biblica Open (Toleo Wazi) License. · Biblica Open License