Zaburi 29

Neno: Kiswahili Contemporary Version

1Mpeni Bwana, enyi mashujaa, mpeni Bwana utukufu na nguvu.

2Mpeni Bwana utukufu unaostahili jina lake; mwabuduni Bwana katika uzuri wa utakatifu wake.

3Sauti ya Bwana iko juu ya maji; Mungu wa utukufu hupiga radi, Bwana hupiga radi juu ya maji makuu.

4Sauti ya Bwana ina nguvu; sauti ya Bwana ni tukufu.

5Sauti ya Bwana huvunja mierezi; Bwana huvunja vipande vipande mierezi ya Lebanoni.

6Hufanya Lebanoni irukaruke kama ndama, Sirioni urukaruke kama mwana nyati.

7Sauti ya Bwana hupiga kwa miali ya umeme wa radi.

8Sauti ya Bwana hutikisa jangwa; Bwana hutikisa Jangwa la Kadeshi.

9Sauti ya Bwana huzalisha ayala, na huuacha msitu wazi. Hekaluni mwake wote wasema, “Utukufu!”

10Bwana huketi akiwa ametawazwa juu ya gharika; Bwana ametawazwa kuwa Mfalme milele.

11Bwana huwapa watu wake nguvu; Bwana huwabariki watu wake kwa kuwapa amani.

Zaburi

Open the interactive reader to switch translations, adjust type, and mark verses — or browse verses by topic.

Neno: Bibilia Takatifu — Kiswahili Contemporary Version. Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015 Biblica, Inc. Used under the Biblica Open (Toleo Wazi) License. · Biblica Open License