Zaburi 7

Neno: Kiswahili Contemporary Version

1Ee Bwana, Mungu wangu, ninakukimbilia wewe, uniokoe na kunikomboa na wote wanaonifuatia,

2la sivyo watanirarua kama simba na kunichana vipande vipande, asiwepo wa kuniokoa.

3Ee Bwana, Mungu wangu, kama nimetenda haya na kuna hatia mikononi mwangu,

4au ikiwa nimemtenda uovu aliye na amani nami, au nimemnyangʼanya adui yangu pasipo sababu,

5basi adui anifuatie na kunipata, auponde uhai wangu ardhini na kunilaza mavumbini.

6Amka kwa hasira yako, Ee Bwana, inuka dhidi ya ghadhabu ya adui zangu. Amka, Mungu wangu, uamue haki.

7Kusanyiko la watu na likuzunguke. Watawale kutoka juu.

8Bwana na awahukumu kabila za watu. Nihukumu Ee Bwana, kwa kadiri ya haki yangu, kwa kadiri ya uadilifu wangu, Ewe Uliye Juu Sana.

9Ee Mungu mwenye haki, uchunguzaye mawazo na mioyo, komesha ghasia za waovu na ufanye wenye haki waishi kwa amani.

10Ngao langu ni Mungu Aliye Juu Sana, awaokoaye wanyofu wa moyo.

11Mungu ni mwamuzi mwenye haki, Mungu aghadhibikaye kila siku.

12Kama hakutuhurumia, atanoa upanga wake, ataupinda na kuufunga uzi upinde wake.

13Ameandaa silaha zake kali, ameweka tayari mishale yake ya moto.

14Yeye aliye na mimba ya uovu na achukuaye mimba ya ghasia huzaa uongo.

15Yeye achimbaye shimo na kulifukua hutumbukia katika shimo alilochimba mwenyewe.

16Ghasia azianzishazo humrudia mwenyewe, ukatili wake humrudia kichwani.

17Nitamshukuru Bwana kwa ajili ya haki yake, na nitaliimbia sifa jina la Bwana Aliye Juu Sana.

Zaburi

Open the interactive reader to switch translations, adjust type, and mark verses — or browse verses by topic.

Neno: Bibilia Takatifu — Kiswahili Contemporary Version. Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015 Biblica, Inc. Used under the Biblica Open (Toleo Wazi) License. · Biblica Open License