Ayubu 35
Neno: Kiswahili Contemporary Version
1Ndipo Elihu akasema:
2“Je, unadhani hili ni haki? Wewe unasema, ‘Nina haki mbele za Mungu.’
3Bado unamuuliza, ‘Ni faida gani nimepata, na imenifaidi nini kwa kutokutenda dhambi?’
4“Ningependa nikujibu wewe pamoja na marafiki zako walio pamoja nawe.
5Tazama juu mbinguni ukaone; yaangalie mawingu yaliyo juu sana juu yako.
6Je, ukitenda dhambi, inamdhuruje Mungu? Kama dhambi zako zikiwa nyingi, hilo linamfanyia nini Mungu?
7Kama wewe ni mwadilifu, unampa nini, au yeye anapokea nini mkononi kwako?
8Uovu wako unamdhuru tu mtu mwingine kama wewe, nayo haki yako inawafaa wanadamu tu.
9“Wanadamu hulia kwa kulemewa na mateso; huomba msaada kutoka mkono wenye nguvu.
10Lakini hakuna asemaye, ‘Yuko wapi Mungu Muumba wangu, yeye anifanyaye niimbe usiku,
11yeye atufundishaye sisi zaidi kuliko wanyama wa dunia, na kutufanya wenye hekima kuliko ndege wa angani?’
12Yeye hajibu wakati watu waliapo kwa sababu ya kiburi cha watu waovu.
13Naam, Mungu hasikilizi maombi yao ya ubatili; Mwenyezi hayazingatii.
14Si zaidi sana kwamba hatakusikiliza wewe usemapo humwoni, tena ya kwamba shauri lako liko mbele zake na wewe lazima umngojee,
15pia zaidi, kwamba hasira yake kamwe haiadhibu wala haangalii uovu hata kidogo?
16Hivyo Ayubu hufumbua kinywa chake kwa maneno yasiyo na maana; anaongea maneno mengi bila maarifa.”
Ayubu
Open the interactive reader to switch translations, adjust type, and mark verses — or browse verses by topic.
Neno: Bibilia Takatifu — Kiswahili Contemporary Version. Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015 Biblica, Inc. Used under the Biblica Open (Toleo Wazi) License. · Biblica Open License