Ayubu 26

Neno: Kiswahili Contemporary Version

1Kisha Ayubu akajibu:

2“Tazama jinsi ulivyomsaidia mtu asiye na uwezo! Jinsi ulivyouokoa mkono ulio dhaifu!

3Ni shauri gani ulilompa yeye asiye na hekima? Nayo ni busara gani kubwa uliyoonyesha!

4Ni nani aliyekusaidia kutamka maneno hayo? Nayo ni roho ya nani iliyosema kutoka kinywani mwako?

5“Wafu wako katika maumivu makuu, wale walio chini ya maji na wale waishio ndani yake.

6Mauti iko wazi mbele za Mungu; Uharibifu haukufunikwa.

7Hutandaza anga la kaskazini mahali patupu; naye huiningʼiniza dunia mahali pasipo na kitu.

8Huyafungia maji kwenye mawingu yake, hata hivyo mawingu hayapasuki kwa uzito wake.

9Huufunika uso wa mwezi mpevu, akitandaza mawingu juu yake.

10Amechora mstari wa upeo juu ya uso wa maji, ameweka mpaka wa nuru na giza.

11Nguzo za mbingu nazo zatetemeka, zinatishika anapozikemea.

12Kwa nguvu zake aliisukasuka bahari; kwa hekima yake alimkata Rahabu vipande vipande.

13Aliisafisha anga kwa pumzi yake; kwa mkono wake alimchoma joka aendaye mbio.

14Haya ni mambo madogo tu katika matendo yake; tazama jinsi ulivyo mdogo mnongʼono tunaousikia kumhusu! Ni nani basi awezaye kuelewa ngurumo za nguvu zake?”

Ayubu

Open the interactive reader to switch translations, adjust type, and mark verses — or browse verses by topic.

Neno: Bibilia Takatifu — Kiswahili Contemporary Version. Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015 Biblica, Inc. Used under the Biblica Open (Toleo Wazi) License. · Biblica Open License